ELIMU

Walimu wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga wamepongezwa kazi nzuri na kupata matokeo mazuri ya shule zao za msingi katika mtihani wa taifa wa mwaka jana.
Pongezi hizo zailitolewa jana na mwakilishi wa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Sigisbert Rwezaula wakati wakati wa hafla ya kupongeza shule kumi zilizofanya vizuri katika mitihani ya mwaka jana.
Katika hafla hiyo iliyofanyika Mwadui wilayani Kishapu ikiambatana na utoaji vyeti kwa walimu wakuu, Rwezaula ambaye alikuwa mgeni rasmi alisema hakuna muujiza wa kufanya vizuri bali ni walimu kujituma.
Aliwataka walimu wakuu wa shule ambazo hazikufanya vizuri kuhakikisha wanaweka mikakati ili ziweze kuibuka vinara kama walivyo wenzao na kuwataka kuendelea kujituma.
”Najua kuna changamoto nyingi kwa walimu kama upungufu au ukosefu wa fedha lakini nawaomba tuvumilie na tukabiliane nazo, jambo kubwa ni kutoa elimu bora kwa wanafunzi wetu na hatimaye wafanye vizuri,” alisisitiza.
Aidha Rwezaula aliongeza kwa kutoa rai kwa walimu wa shule hizo za msingi zilizopo katika halmashauri hiyo kuwa na utamaduni wa kujiendeleza kimasomo ili kukabiliana na changamoto mbalimbali.
Alisema hivi sasa dunia ipo katika utandawazi ambapo kunashuhudiwa ugunduzi mkubwa wa kiteknolojia ambao unahitaji maarifa makubwa ili kuendesha masuala mbalimbali ya kitaaluma.
”Ni vizuri walimu mkajiendeleza kielimu msiishe hapo mlipo, msikubali kuwa nyuma ya wakati kwani hivi sasa elimu ni muhimu sana na mnashuhudia dunia ni kama kijiji mnaweza kupata habari kwa mitandao,” alisema.  
Rwezaula aliwataka kuwa na utaratibu wa kufidia vipindi vilivyopotea wakati mwalimu kapata dharura au ruhusa na kushindwa kuingia darasani na kuwafundisha wanafunzi.
Alisema kwa kuwa na utaratibu huo kutawawezesha wanafunzi kupata wasaa wa kujifunza na kuelewa masomo yao kwa wakati na hivyo kufanya vizuri zaidi kwenye mitihani yao.
Awali wanataaluma hao walifanya kikao kazi cha kutathmini mambo yaliyojiri kitaaluma katika Idara ya Elimu Msingi halmashauri ya wilaya hiyo kipindi cha mwaka 2016.
Kikao hicho kilichofanyika Mwadui kilihusisha maofisa elimu msingi, waratibu elimu kata, walimu wakuu na badhi ya walimu wa shule mbalimbali za msingi zilizopo Wilaya ya Kishapu    


 
Afisa Elimu Msingi Mwl Sosthenes Mbwilo akitoa nasaha katika hafla hiyo