Monday, April 3, 2017

NAIBU WAZIRI WA NISHATI AZINDUA MRADI WA UMEME VIJIJINI

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk. Medard Kalemani akibonyeza kitufe cha kifaa cha umeme kama ishara ya uzinduzi wa mradi wa kusambaza umeme vijijini awamu ya tatu katika mkoa wa Shinyanga wilayani Kishapu wenye thamani ya sh. bilioni 35.5.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk. Medard Kalemani amezindua mradi wa kusambaza umeme vijijini awamu ya tatu katika mkoa wa Shinyanga wilayani Kishapu wenye thamani ya sh. bilioni 35.5.
Katika uzinduzi huo uliofanyika kijiji cha Negezi kata ya Ukenyenge wilayani Kishapu,ukihusiha vijiji 149, Dk. Kalemani aliagiza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kuhakikishwa wanasambaza umeme sehemu zote bila upendeleo.
Aliwahimiza wananchi kutumia fursa ya kuwepo kwa nishati hiyoi katika kuboresha maisha yao kwa kutumia miradi ya uzalishaji mali pamoja na huduma mbalimbali za kijamii.
Aliwataka wautumie kwa kujenga viwanda vya kusindika mazao pamoja na huduma za afya, elimu, maji na viwanda vingine kama mashine za kusaga ambazo zitawapatia kipato  na kuboresha maisha.
Aidha, naibu waziri huyo alizitaka serikali za kata na vijiji kubainisha maenbeo maalumu ya viwanda ambayo katika mradi huo yatafikishiwa miundombinu ya umeme mkubwa.
”Tunataka kuwezesha wajasriamali vijijini kupatiwa umeme utakaowezseha kuanzishwa kwa viwanda vidogo na vikubwa vijijini kwa gharama nafuu,” alisema Dk. Kalemani.
Aliongeza kuwa wananchi watakaounganishiwa umeme wanatakiwa kukamilisha utandazaji wa nyaya katikia nyumba zao mapema ili mkandarasi akifika wawe tayari kulipia na kuunganishiwa umeme.
Alisema kwa sehemu ambazo utandazaji utakuwa haujakamilika au nyumba si kubwa wanahimizwa kuomba kufungiwa kifaa cha Umeme Tayari (UMETA) ambacho hakihitaji kutandaza nyaya.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Taraba aliishukuru Serikali kwa mradi huo wa REA huku akisema utasaidia kutengeneza ajira wilayani humo.
Taraba akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack alisema nishati ya umeme vijijini itasaidia kuanzishwa kwa viwanda vidogo na vya kati hivyo aliwataka wananchi kutumia fursa hiyo na kuacha uharibifu wa mazingira.
Hata hivyo, alitoa kilio chake kwa kumuomba naibu waziri kushughulikia changamoto ya baadhi ya wakandarasi kutomaliza miradi kwa wakati jambo ambalo linarudisha nyuma maendeleo.
Pia mkuu huyo wa wilaya aliwaomba wananchi watoe ushirikiano kwa kutoa maeneo kwa ajili ya kupitisha miundombinu ya umeme kwa kuwa ni kujiletea maendeleo yao wenyewe.
 Aliomba Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) Mkoa wa Shinyanga kutatua kero ya kukatika kwa umeme mara kwa jambo ambalo limekuwa ni kero kwa wananchi na linarudisha nyuma maendeleo.

Utekelezaji wa mradi huo ulianza Februari 2017 na unatarajiwa kukamilika Machi 2019 ambapo tayari sh. bilioni 7.4 zimetumika katika awamu ya kwanza wakati awamu ya pili jumla ya sh. bilioni 22.95 zilitumika.