Wednesday, May 2, 2018

Chajo ya kuzuia Saratani ya Mlango wa Kizazi yazinduliwa rasmi Chalinze


Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo,Alhaj Majid Mwanga amezindua rasmi kampeni ya chanjo ya kuzuia Saratani ya Mlango wa Kizazi kwa watoto wa kike waliofikia umri wa miaka 14,uzinduzi huo umefanyika jana katika kijiji cha Kikaro kata ya Miono katika halmashauri ya wilaya ya Chalinze.Kampeni hizi ni mkakati wa serikali ya awamu ya tano katika kupambana na ugonjwa wa saratani ya mlango wa kizazi ambao umekuwa tishio kwa afya za wanawake hapa nchini na ulimwenguni kote kwa ujumla.

Mkuu wa wilaya ya Bagamoyo Majid Mwanga akizindua zoezi la chanjo ya kuzuia saratani ya mlango wa kizazi

Shehe Hamis Nasoro akichangia jambo katika uzinduzi wa

Wanafunzi wa shule ya sekondari Kikaro

Shehe akihamasisha zoezi la chanjo



Kabla ya uzinduzi wa kampeni hiyo kulitolewa mafunzo kwa wadau na wahamasishaji wa masuala ya afya ya msingi katika jamii kwa maana ya wahudumu wa afya,maafisa watendaji wa vijiji na kata,maafisa tarafa,maafisa maendeleo ya jamii,viongozi mbalimbali wa dini na walimu wa shule za msingi na sekondari ili wapate ufahamu kuhusu saratani ya mlango wa uzazi,dalili za maabukizi ya virusi vya “Human Pappiloma Virus”(HPV),dalili za saratani ya mlango wa kizazi,chanjo ya kukinga Saratani ya mlango wa kizazi,namna inavyotolewa chanjo na maudhi madogo madogo yanayoweza kutokea baada ya chanjo kwa watoto.
Katika mafunzo hayo Mganga Mkuu wa halmashauri ya wilaya Dkt.Rahim Hangai aliwataka washiriki kuwa mabalozi katika kufanikisha zoezi hili muhimu la kitaifa ili kuwanusuru watoto wa kike wasipatwe na virusi vya HPV na kupelekea kupatwa na saratani ya mlango wa kizazi ugonjwa ambao ni hatari na unaua wanawake wengi katika nchi zinazoendelea.
Naye Mratibu wa chanjo wa wilaya Ally Msopa,akitoa mada kwa washiriki aliwaeleza umuhimu wa chanjo ya HPV kuwa inakinga maambukizi ya virusi vya HPV vinavyosababisha saratani ya mlango wa kizazi na inatolewa mara mbili ili kupata kinga kamili,chanjo hii inaweza kupunguza matukio ya saratani ya mlango wa kizazi kwa kiwango kikubwa.Chanjo hii ni salama,imethibitishwa na Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Wazee na Watoto na Shirika la afya Duniani.
Aidha Msopa alifafanua baadhi ya dalili za awali  za maabukizi ya virusi vya HPV kuwa ni vivimbe sehemu za uke au uume vijulianavyo kama viotea,dalili za baadaye ni mabadiliko katika seli za mlango wa kizazi na mabadiliko haya yasipodhibitiwa mapema hugeuka kuwa saratani ya mlango wa kizazi au viungo vingine.
Kwa upande wake kiongozi wa dini ya kiislamu Sheikh Hamis Nassor kwa niaba ya viongozi wa dini alisema tumepokea mkakati huu wa serikali kwa mikono miwili tutahamasisha jamii kwa nguvu zote ili kuwanusuru mabinti zetu na janga la saratani ya mlango wa kizazi, na kila changamoto itakayojitokeza tutakabiliana nayo.”Naomba Mungu awajalie viongozi wetu afya njema umri wenye tija katika kulitumikia taifa”.Sheikh Nassor alisema.
Mkuu wa wilaya katika hotuba yake ya uzinduzi wa kamapeni ya chanjo ya kuzuia Saratani ya Mlango wa Kizazi aliwataka watumishi wa idara ya afya kuwa na moyo wa uzalendo na wa kujitolea ili zoezi hili liweze kufanikiwa kwani kuna zahanati ambazo hazina watumishi wa afya na vijiji vingine havina kabisa zahanati, hivyo alimtaka Mganga wa Halmashauri kuendesha zoezi hili kwa njia ya huduma ya Vikoba (Out Reach Services)kwa kupanga ratiba za kuwafikia wananchi katika maeneo yao kwa muda mahsusi ili tuweze kukamilisha zoezi hili kwa asilimia 100.Baada ya nasaha zake alizindua rasmi kampeni ya chanjo kwa watoto wa kike wote waliofikia umri wa miaka 14.