Tuesday, June 6, 2017

Shinyanga waadhimisha Siku ya Mazingira kimkoa wilayani Kishapu



Mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Zainab Telack ameagiza wananchi kuendelea kuelimishwa kuhusu athari zinazotokana na vitendo vya ukataji miti ovyo.
Alitoa agizo hilo juzi katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mkuu wa wilaya ya Kishapu, Nyabaganga Talaba wakati wa kilele cha Wiki ya Mazingira Duniani iliyoadhmishwa kimkoa kijiji cha Mwamashele wilayani hapa.
Alisema wananchi wengi wanakosa uelewa kuwa vitendo vya ukataji miti vinatishia uhai wa binadamu na wanyama hali inayotokana na ukosefu wa mvua na hivyo kusababisha ukame.
Telack alifafanua kuwa misitu ndiyo mhimili mkubwa wa kulinda mazingira yetu na kutupatia nishati, dawa za asili, vifaa vya ujenzi pamoja na kuboresha hali ya hewa.
“Pamoja na umuhimu wake kwa binadamu na mazingira misitu imekumbwa na uharibifu mkubwa katika mkoa wetu wa Shinyanga kwa matumizi mbalimbali yakiwemo ya uchomaji mkaa,” alisema.
Mkuu huyo wa mkoa aliongeza kuwa uchomaji wa mkaa katika maeneo mengi kama vile Nyasamba wilayani hapa umekuwa kama shughuli ya kujipatia kipato na hivyo kutishia kutoweka kwa misitu.
Hivyo aliwataka wadau kutumia nishati mbadala kama vile vinyeshi vya wanyama pamoja na kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi hayo kwani matumizi ya mkaa ni adui wa mazingira.
Telack alionya kuwa uchomaji mkaa na utumiaji wake huongeza hewa ya ukaa na kusababisha mabadiliko ya tabia ya nchi na hatimaye kuleta ukame.